Umuhimu wa kulinda nidhamu ya kijamii na mchango wa mwanchuoni katika hilo

| |times read : 758
Umuhimu wa kulinda nidhamu ya kijamii na mchango wa mwanchuoni katika hilo
  • Post on Facebook
  • Share on WhatsApp
  • Share on Telegram
  • Twitter
  • Tumblr
  • Share on Pinterest
  • Share on Instagram
  • pdf
  • Print version
  • save

Umuhimu wa kulinda nidhamu ya kijamii na mchango wa mwanchuoni katika hilo

Kwa jina la Mwenyezi Mungu Mtukufu:

Maulama wengi wamekuwa wakikariri sana anuani ya “...Kuhifadhi nidhamu ya kijamii..” huku wakitoa dalili kwa kutegemea baadhi ya hukumu ambazo ni shamili. Lakini anuani hii haikuthibiti katika riwaya tukufu, isipokuwa tu maulama wameitumia kama anuani mama katika kuashiria mkusanyiko wa maslahi pamoja na taasisi zenye kusimamia maslahi ambayo sheria imeyatilia mkazo mno, kwa sababu ndani yake kuna jambo la kupangilia maisha ya watu ikiwa ni pamoja na kutengeneza miji yao, kuleta amani na utulivu ndani ya miji hiyo.

Na umuhimu huu unaonekana wazi kabisa katika riwaya nyingi mno na hata vitabu vingi vya kifiqhi kama vile vitabu mahususi kwa mambo ya ardhi na mashamba, yanayofaa na yasiyofaa kuchumwa, kukataza mabaya na kuamrisha mema, na hata katika hukumu ambazo ni shirikiana kama vile zenye kuhusu maji na mali na mengineyo mengi. Lakini maulama hawajanakili makusudio ya hukumu hizi katika nyanja za siasa, uchumi na jamii au maswala ya kuendesha miji, bali unakuta imebakia tu katika tungo na vitabu vya kifiqhi, hata kama asili ya mafunzo yake bado yapo katika akili za maulama, na ndio hiyo wanayosema ni kuhifadhi nidhamu ya kijamii kwa ujumla. Tunataraji katika kizazi hichi kilicho makini kuweza kuchambua hizi nidhamu za Kiislamu na kuziweka sawa katika milango yake tofauti tofauti.

Na utakuta dalili kama vile dalili yenye kulinda heshima ya mwanadamu au dalili za kumpwekesha Mwenyezi Mungu ni dalili zenye kuhukumu hata katika maswala mengine, kama vile kutengeneza katiba ambayo itakuwa ndio msingi wa kanuni nyingine, kiasi kwamba haitatoa nafasi yeyote ya kuwepo kwa kanuni itakayopingana na katiba ile.

Mfano itakapotokea kwamba kuna mradi wa dharura kwa maisha ya watu kama vile kutengeneza barabara, na ikawa inategemea kujimilikisha baadhi ya mali za watu ambao hawataki kuuza mali zao, hapa Faqihi atatoa hukumu ya kumilikisha mali hizi kwa nchi na kuchukua kwa mmiliki wake haki ya kubakia nayo ikiwa ni pamoja na kumpatia thamani inayoendana na mali ile. Na ndio maana unakuta kwamba jambo la kwanza ambalo Imamu Ally alilifanya baada ya kuchukua dola ni kujaribu kurudisha ardhi zote ambazo Othman alizigawa kwa watu wake wa karibu au baadhi ya watu bila kuzingatia haki, kwani ni katika mali za umma ambazo hakuna mwenye haki ya kuzimiliki tofauti na kunufaisha umma.

Sasa uwepo wa misingi kama hii ni dalili tosha ya kwamba Uislamu ni dini ya dola, uadilifu pamoja na kutengeneza jamii iliyo na furaha na utulivu, na si dini ya kujitenga na kukamuana. Na ndio maana hukumu zake zinaangalia kila sababu na vyanzo kwa ajili ya kusimamisha dola nzuri pamoja na kumjenga mwanadamu huru na mwema.

“...Yeye ndiye ambaye amewatoa kutoka ardhini na kisha kuwaweka humo...”[1]

Pia katika majukumu yake ni kujaribu kutoa kila vizuizi vyenye kuzuia kukamilika kwa jambo hilo. Mwenyezi Mungu anasema “...Na kwa hakika tumemtukuza mno mwanadamu...”[2]

Na hapa ndio utakuta kwamba moja ya mambo ya haramu na mazito zaidi katika Uislamu ni jambo la kuharibu nidhamu ya kijamii, kuharibu taasisi zenye kusimamia maswala ya miji, kuleta fujo, kusababisha hofu katika nyoyo za watu, na kuondoa utulivu na amani yao, kwani katika kufanya hivyo ni kufanyia uadui yale matakwa ya Mwenyezi Mungu (swt).

Pia ukirejea utakuta Maimamu walikuwa wakiwajenga sana masahaba wao katika kuweza kutofautisha baina ya Dola na Utawala, kwa maana ya kwamba kupinga Tawala za kidhalimu na kutotambua uhalali wake hakuendani kabisa na kuharibu au kufanyia uadui taasisi ambazo zinafanya kazi ya kusimamia huduma za kijamii kama vile afya, elimu, mipango miji na njia zake, ulinzi wa mipaka, usalama wa ndani ikiwa ni pamoja na machumo ya watuna mengineyo, abadan Maimamu hawakuwa radhi na mambo kama haya. Bali walikuwa katika mustawa wa juu sana katika kuhisi kwamba wana majukumu ya kuwa na adabu zenye kusifika, kwani hata katika wakati ambao watawala wa kidhalimu walikuwa wakija na kila aina ya vitisho bado unakuta Maimamu walikuwa ni wenye nia ya kuhifadhi maslahi ya kijamii na nidhamu yake kwa ujumla.

Mengi sana nimeyataja katika kitabu changu cha “Mchango wa Maimamu katika maisha ya Kiislamu..”, mfano ambavyo Imamu Sajjad alisimama kidete katika kuhakikisha kwamba Dola ya Kisalamu inakuwa na sarafu yake  na kisha kumpatia Abdul Malik bin Marwan baada ya Mfalme wa Roma kutishia ya kwamba sarafu yake ndiyo yenye kutawala.

Au dua yake alipowaombea wanajeshi wenye kulinda mipaka ya Kiislamu pia ni dalili nyingine katika hili. Pia kabla ya hapo utakutana na nasaha kutoka kwa Imamu Ally (as) kwa watawala ambao walimtangulia, na pia kuna dalili nyingine nyingi mno.

Na kwa ajili ya umuhimu wa maswala kama haya, unakuta Mwenyezi Mungu amemfanya Faqih mwenye kutimiza vigezo vyote, awe ndio mtawala wa mambo yote, kwani huyu ndio ana uwezo wa kuchagua misimamo sahihi kutokana na elimu na upeo wake alio nao.

Na tumeeleza katika sehemu nyingine hapo kabla, kwamba hata huyu Faqih pia anakuwa ndani ya Demokrasia, kwani anaweza kutengua baadhi ya hukumu za kibinadamu ima kwa kuamrisha au kushauri au kuelekeza, na hii ni kwa kuwa yeye ndiyo muhifadhi wa kwanza wa mambo ya watu. Kwa mfano Bunge litakapopitisha kanuni ambayo Faqih akaona kuna hali ya kukiuka baadhi ya haki za binadamu, anaweza kuivunja na wala hakuna mwenye haki ya kufanyia kazi hukumu ile eti kwa kuwa tu imepitishwa na wengi, na mfano mwingine wa hayo.

Kama vile Bunge litakapojipa nafasi za juu zaidi pamoja na watumishi wa nchi, kitendo hichi si cha kisheria kabisa, achilia mbali njia nyingine ambazo si za kikanuni katika kujimilikisha mali za Umma.

Ayatollah Muhammad Yaaqubiy

21 Shaaban 1438

18/5/2017



[1] Surat hud aya 61

[2] Surat Israa aya 70